15/09/2026
TANZANIA NA JAPAN KUIMARISHA USHIRIKIANO WA UWEKEZAJI
Ujumbe wa maafisa kutoka taasisi zinazosimamia uwekezaji nchini, ikiwemo Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA) na Ubalozi wa Tanzania nchini Japan, umeendelea na ziara yake katika Mji wa Okinawa, Japan, kwa lengo la kujifunza uzoefu na kutambua fursa za ushirikiano wa uwekezaji kati ya Tanzania na Japan, hususan Zanzibar.
Ziara hiyo imeandaliwa kwa pamoja na ZIPA, TISEZA na Ubalozi wa Tanzania nchini Japan, ikiwa na lengo la kuimarisha uhusiano kati ya taasisi za umma na sekta binafsi, pamoja na kuchunguza maeneo ya ushirikiano yanayoweza kuchangia maendeleo endelevu ya uchumi wa visiwa.
Katika ziara hiyo, ujumbe wa Tanzania umefanya mazungumzo na Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA) Okinawa, ambapo walijadili fursa za kujenga uwezo, uhamishaji wa maarifa na teknolojia, kuimarisha taasisi na kubadilishana uzoefu katika maendeleo ya uchumi wa visiwa.
Aidha, ujumbe huo ulitembelea Ryukyu Mura, eneo linaloonesha utamaduni na urithi wa jadi wa Okinawa, na kujifunza namna utamaduni, usanifu wa majengo, sanaa za mikono na urithi wa jamii vinavyoweza kutumika katika kukuza utalii na uchumi wa ndani.
Ziara hiyo imetoa maarifa muhimu kwa Tanzania, hususan Zanzibar, kuhusu namna ya kuunganisha utamaduni, urithi, ushiriki wa jamii na biashara za ndani katika uwekezaji wa utalii, huku ukihifadhi utambulisho wa maeneo husika.
Mbali na utalii, ziara hiyo inahusisha maeneo mengine ya kimkakati, yakiwemo uchumi wa buluu, uvuvi na ufugaji wa viumbe vya majini, elimu na utafiti, teknolojia na maendeleo endelevu ya uchumi wa visiwa.
Kupitia ziara hiyo, ZIPA, TISEZA na Ubalozi wa Tanzania nchini Japan wanaendelea kuwezesha ushirikiano wa Tanzania na Japan katika uwekezaji, uhamishaji wa teknolojia na maarifa, pamoja na kuimarisha mahusiano kati ya wafanyabiashara na taasisi za nchi hizo mbili.