19/09/2026
PROF. MUSHI: IPOSA IWE DARAJA LA KUUNGANISHA VIJANA NA ELIMU, AJIRA
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi, amezitaka Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW), Halmashauri na wadau mbalimbali kuendelea kuimarisha utekelezaji wa Programu ya Elimu Changamani kwa Vijana Walio Nje ya Mfumo Rasmi wa Elimu (IPOSA) ili iwe daraja la kuwaunganisha vijana na elimu zaidi, ajira na maisha bora.
Prof. Mushi ametoa kauli hiyo, Septemba 18, 2026, mkoani Tanga, akimwakilisha Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, katika hafla ya uzinduzi rasmi wa Programu ya IPOSA awamu ya Pili (IPOSA II).
Amesema IPOSA II ni utekelezaji dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata fursa ya elimu bila kujali umri, mahali alipo au changamoto alizokutana nazo.
Ameelekeza TEWW kuimarisha ushirikiano na VETA, SIDO, FDC na sekta binafsi kwa kuunganisha mafunzo ya IPOSA na mafunzo kwa vitendo, ushauri wa kitaalamu, ziara za kujifunza pamoja na fursa za ajira.
Prof. Mushi amesema mafanikio yaliyopatikana katika mikoa sita inayotekeleza IPOSA II kwa ufadhili wa Serikali ya Korea Kusini kupitia KOICA yanapaswa kuwa msingi wa kuimarisha utekelezaji wa programu hiyo katika mikoa mingine kwa kuzingatia ubora wa mafunzo, upatikanaji wa wawezeshaji wenye sifa na usimamizi madhubuti.
Amesema Serikali inatambua mchango wa Serikali ya Korea Kusini kupitia KOICA katika kuimarisha utekelezaji wa IPOSA na amepongeza wadau mbalimbali walioshiriki katika programu hiyo,
Naye Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania, Balozi Eunje Ahn amesema Serikali ya Korea Kusini kupitia KOICA imetoa takribani dola za Marekani milioni sita kwa ajili ya utekelezaji wa programu hiyo katika mikoa sita ya Pwani, Shinyanga, Simiyu, Lindi, Tanga na Manyara.
Amesema kupitia mradi huo, jumla ya vituo 31 vimejengwa, vikiwemo vituo vitatu vya mfano vilivyopo Shinyanga, Manyara na Tanga, pamoja na kituo kimoja maalumu kilichopo Tanga pamoja na kutoa vifaa na kujengea uwezo wawezeshaji.