18/09/2026
NAIBU WAZIRI QWARAY ASISITIZA UTUNZAJI WA MIRADI YA TASAF
Na. Antonia Mbwambo na Helela Lusungu – Geita
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray, amesisitiza umuhimu wa kutunzwa na kutumiwa ipasavyo miradi inayotekelezwa kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) ili iweze kutoa huduma endelevu na kunufaisha wananchi.
Mhe. Qwaray ametoa kauli hiyo alipofanya ziara ya kutembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa kupitia TASAF katika Mkoa wa Geita, ikiwemo Mradi wa Ujenzi wa Jengo la Utawala katika Shule ya Sekondari Fazilibucha, iliyopo Kata ya Bombambili, Manispaa ya Geita.
Aidha, Mhe. Qwaray ametembelea na kukagua Mradi wa Ujenzi wa Jengo la Huduma za Wagonjwa wa Nje (OPD) pamoja na jengo la Huduma za Afya ya Uzazi na Mtoto (RCH) katika Zahanati ya Kakora, iliyopo Kijiji cha Kakora, Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale, Mkoa wa Geita.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Qwaray amesema kuwa uwekezaji unaofanywa na Serikali kupitia TASAF ni kwa ajili ya kuboresha huduma za kijamii na kuinua ustawi wa wananchi, hivyo ni wajibu wa viongozi na Wananchi kuhakikisha miradi hiyo inatunzwa na kutumika kwa madhumuni yaliyokusudiwa.
“Miradi hii ni mali ya wananchi na imejengwa kwa lengo la kuwapatia huduma bora na endelevu. Ni muhimu kuhakikisha inatunzwa vizuri, inatumika ipasavyo na kila mmoja anawajibika kulinda uwekezaji huu ili uweze kunufaisha jamii.” – Mhe. Qwaray amesema.
Ameongeza kuwa utunzaji wa miundombinu hiyo utasaidia kuongeza muda wa matumizi ya majengo na kuhakikisha Wananchi wanaendelea kupata huduma muhimu za kijamii bila kulazimika kutumia rasilimali nyingi katika ukarabati wa mara kwa mara.
Amesema Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa kuhakikisha inakamilika kwa wakati, inazingatia viwango vinavyohitajika na inatumika kwa manufaa yaliyokusudiwa.