20/05/2026
KATA 30 WILAYANI SERENGETI ZANUFAIKA NA MILIONI 88 ZA MFUKO WA JIMBO.
Mbunge Jimbo la Serengeti Mhe. Mary Daniel Surati leo Mei 20, 2026 amefanya hafla ya mgawanyo wa fedha za mfuko wa Jimbo Shilingi Milioni 88 kwa Kata 30 za Wilaya ya Serengeti.
Hafla hiyo iliyofanyika katika Viwanja vya Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti na kushuhudiwa na Madiwani wa kata zote pamoja wananchi, imehusisha ugawaji wa mifuko 2597 ya saruji ikiwa ni fedha za mfuko wa j
Jimbo na mchango wa mifuko 500 ya saruji kutoka Taasisi ya Nyansaho (Nyansaho Foundation), Hundi ya Shilingi Milioni 25 kwa ajili ya ukamikishaji wa Zahanati ya Kisaka sambamba na madawati yenye thamani ya Shilingi Milioni 2 kwa Shule ya Msingi Kambarage.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo Mhe. Mary amesisitiza kuwa, lengo la mgawanyo wa fedha hizo ni kuhakikisha kuwa miradi yote ya elimu na afya katika Kata zote za Wilaya ya Serengeti inakamilika ili wananchi waweze kuondokana na adha ya kutembea umbali mrefu kupata huduma za elimu na afya.
Sambamba na hayo ameongeza kuwa kipaumbele cha Serikali ya awamu ya sita ni kuwajali wananchi wake ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma bora za muhimu katika maeneo yao huku akiwasisitiza Waheshimiwa Madiwani kuhakikisha wanasimamia matumizi sahihi ya saruji hiyo na fedha.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Serengeti Mhe. Wakili Angelina Marco Lubella amemshukuru Mbunge wa Jimbo la Serengeti kwa uwazi wake katika mgawanyo wa fedha za mfuko wa jimbo huku akimhakikishia usimamizi mzuri wa fedha hizo ili ziweze kutimiza lengo lililokusudiwa.
Nao Waheshimiwa madiwani wamepongeza hatua ya Mbunge huyo kwa uamuzi wa kutoa mifuko hiyo ya saruji na fedha kwani inaenda kukamilisha miradi mbalimbali iliyokuwa imekwama katika kata zao.