13/09/2026
MEYA TANGA AIPONGEZA NHC KWA MKWAKWANI PLAZA, ATAKA UWEKEZAJI MKUBWA ZAIDI
Meya wa Jiji la Tanga, Mustafa Selebos, ameipongeza NHC kwa jitihada na kasi ya ujenzi wa Mkwakwani Plaza, akisema mradi huo umekuja wakati muafaka kutokana na ukuaji wa shughuli za kiuchumi na ongezeko la mahitaji ya majengo ya kisasa ya makazi na biashara jijini Tanga.
“Kwanza niwashukuru sana watu wa NHC kwa jitihada zao na kasi yao. Kwa kweli kasi hii imeendana na uhitaji uliopo. Ukiangalia Mkwakwani Plaza sasa, jengo limefikia hatua za mwisho kabisa, jambo ambalo linatia moyo,” amesema Selebos.
Amesema kukua kwa shughuli za Bandari ya Tanga na kuongezeka kwa wageni wanaoingia jijini humo kwa shughuli za biashara na uwekezaji kunazidi kuongeza mahitaji ya nyumba za kisasa pamoja na maeneo bora ya kufanyia biashara.
Kwa mujibu wa Meya huyo, hali hiyo inatoa sababu zaidi kwa NHC kuendelea kutafuta maeneo mengine yenye fursa na kufanya uwekezaji mkubwa zaidi ili kwenda sambamba na mabadiliko ya kiuchumi yanayotokea Tanga.
“Hivyo, kwa NHC naona ipo haja ya kufanya uwekezaji mkubwa zaidi ya huu wa Mkwakwani Plaza. Tanga inafunguka, shughuli za kiuchumi zinaongezeka na watu wanaingia kwa ajili ya fursa mbalimbali. Hii maana yake ni kwamba mahitaji ya nyumba za kisasa na maeneo ya biashara yataendelea kuongezeka,” amesema.
Ameongeza kuwa Mkwakwani Plaza yenyewe imewekwa katika eneo la kimkakati katikati ya Jiji la Tanga, lenye muunganiko mzuri wa barabara zinazoelekea maeneo mbalimbali. Upande wa kaskazini kuna njia inayoelekea Mombasa, huku upande wa kusini kukiwa na njia ya Pangani inayounganisha maeneo yanayoelekea Dar es Salaam.
Kwa mtazamo wake, uchaguzi wa eneo hilo unaonesha namna wataalamu, wahandisi na Menejimenti ya NHC walivyotambua mapema uwezo wa eneo hilo katika biashara na uwekezaji.
“Hii inaonesha kwamba wenzetu wa NHC wamepeleka kitega uchumi katika eneo lenye potential kubwa. Wataalamu, wahandisi na Menejimenti yao wamefikiria vizuri eneo hili, na ninaamini uwekezaji huu utakuwa na ushindani mkubwa. Tunachotamani sasa ni kuona NHC ikiendelea kuwekeza zaidi Tanga,” amesema Selebos.
Mkwakwani Plaza ni mradi wa NHC wa matumizi mchanganyiko unaolenga kutoa